Obama alaani utamaduni wa ghasia za bunduki
- 29 Novemba 2015
Rais wa Marekani Barack Obama ameshutumu utamaduni wa ghasia za bunduki baada ya watu watatu kuuawa katika shambulio lililofanywa kwenye kliniki moja ya mpango wa uzazi katika jimbo la Colorado.
Obama alisema kuwa hali hiyo imetosha sasa nchini Marekani na kuwa lazima wananchi wachukue hatua kuhakikisha kuwa watu hawapati bunduki kwa urahisi nchini humo.
Obama alisema kuwa mtu aliyefyatuliana risasi na polisi kwa saa kadhaa alikuwa akitumia bunduki ambayo kwa kawaida hutumiwa na wanajeshi.
Raia wawili na afisa mmoja wa polisi walifariki katika makabiliano hayo ingawa hadi sasa lengo la mashambulizi hayo halijulikani.
Wakati huohuo habari zaidi zimefichuka kuhusiana na mtu huyo aliyeshambulia kituo hicho cha upangaji wa uzazi.
Robert Dear, mwenye umri wa miaka 57, ametajwa na watu wanaomjua kama mtu anayependa kutembea pekee yake na ambaye hugombana na majirani wake na polisi mara kwa mara.
Aidha polisi wanasema kuwa Robert alipiga mayowe akisema hataki kuendelea kuwepo kwa miili ya watoto akiashiria mbinu ya kuwasaidia watu kupanga familia zao.
Yamkini bwana huyo ambaye anadaiwa kuwa mtu mpweke na anapinga vikali haki ya kuavya mimba.